
BOOK OVERVIEW
Maji Hayafuati Mkondo ni riwaya ya kipekee iliyoandikwa na mwandishi wa kike Felista Richard Mhonge . Riwaya hii inazungumzia changamoto anazokumbana nazo mwanamke katika kufikisha ndoto za maisha yake. Mama Sinta, Sinta na Mercy ni wahusika ambao mwandishi anawatumia katika kuonesha mchango wa mwanamke katika kujenga familia kimaadili na kiuchumi. Wahusika hawa wanachorwa na mwandishi kama wanawake wenye utashi mkubwa wa kupambanua mambo pamoja na ujasiri mkubwa katika kupambana na changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika maisha yao. Kwa kutumia wahusika hawa na wengine, mwandishi anasisitiza suala la umuhimu wa wazazi kushiriki kwa pamoja katika kulea watoto na kujenga familia kwani ndio mhimili wa taifa lenye uadilifu. Mwandishi anapiga vita wazazi na walezi ambao wanashiriki kwa makusudi katika kuangamiza kizazi kipya. Anakemea suala la matumizi ya madawa ya kulevya, biashara ya binaadamu pamoja na rushwa. Mwandishi anaonesha pia umuhimu wa vyombo vya dola katika kusimamia haki za wanaodhulumiwa katika jamii.